Skip to main content
๐Œ๐Š๐„๐๐˜๐€ ๐€๐Ž๐Œ๐๐€ ๐’๐‡๐„๐‘๐ˆ๐€ ๐ˆ๐‘๐„๐Š๐„๐๐ˆ๐’๐‡๐–๐„ ๐Š๐”๐–๐€๐“๐€๐Œ๐๐”๐€ ๐‘๐€๐’๐Œ๐ˆ ๐–๐€๐™๐„๐„ ๐–๐€๐’๐ˆ๐Œ๐€๐Œ๐ˆ๐™๐ˆ ๐–๐€ ๐Œ๐ˆ๐“๐€๐€.

๐Œ๐Š๐„๐๐˜๐€ ๐€๐Ž๐Œ๐๐€ ๐’๐‡๐„๐‘๐ˆ๐€ ๐ˆ๐‘๐„๐Š๐„๐๐ˆ๐’๐‡๐–๐„ ๐Š๐”๐–๐€๐“๐€๐Œ๐๐”๐€ ๐‘๐€๐’๐Œ๐ˆ ๐–๐€๐™๐„๐„ ๐–๐€๐’๐ˆ๐Œ๐€๐Œ๐ˆ๐™๐ˆ ๐–๐€ ๐Œ๐ˆ๐“๐€๐€.

Mkenya Benson Nyaga Kagete amefika mbele ya Kamati ya Kudumu ya Usalama wa Taifa, Ulinzi na Uhusiano wa Kigeni kwenye Bunge la Seneti Alhamisi hii kulitetea ombi lake la kutaka Wazee Wasimamizi wa Mitaa watambuliwe rasmi na serikali na kulipwa chini ya mfumo wa Nyuma Kumi.

Nyaga akiwa mbele ya Kamati hiyo inayoongozwa na Seneta wa Kaunti ya Baringo William Cheptumo alisema Wazee Wasimamizi wa Mitaa wanatekeleza wajibu muhimu katika utendakazi wa Serikali ya Kitaifa katika kiwango cha kijiji kwa kuwasaidia Machifu na Manaibu wao kudumisha sheria na amani, kukuza elimu na maendeleo kupitia kwa mfumo wa Nyumba Kumi.

Alisema inasikitisha kwamba Wazee hao hutekeleza wajibu huo pasi na mshahara wala malipo yoyote jambo alilosema linawavunja moyo pakubwa.

โ€œHamna sheria wala kanuni ambazo zinaweka mwelekeo wa kuwaajiri na kuwakumbatia Wazee Wasimamizi wa Mitaa kwenye Mfumo wa Utawala uliopo kwa sasa,โ€ alifafanua Mlalamishi.

โ€œSheria ya Usimamizi wa Serikali ya Kitaifa Nambari 1 ya mwaka 2013 haielezei kijiji kuwa sehemu ndogo zaidi ya utawala baada ya kata ndogo,โ€ alikariri Nyaga.

Mlalamishi huyo anasema pana haja ya kuweka utaratibu wa kubuni kijiji kuzingatia idadi ya watu, upana wa eneo na masuala ya kijamii na kiutamaduni.

Kwenye ombi lake, Nyaga anataka Sheria ya Usimamizi wa Serikali ya Kitaifa Nambari 1 ya mwaka 2013 kufanyiwa marekebisho ili kujumuisha kijiji kuwa sehemu ndogo ya utawala baada ya kata ndogo na kubuni Baraza la Kijiji.

Aidha Mlalamishi huyo aliliomba Bunge la Seneti kuishinikiza Wizara ya Usalama wa ndani na Utawala wa Taifa kubuni sera kabambe ya uajiri na ujira kwa Wazee Wasimamizi wa Mitaa hususan sera hiyo iangazie masharti ya kufanya kazi, majukumu ya Wazee hao, mfumo wa kuwaajiri na kusitisha utendakazi wao.

Maseneta wanachama wa Kamati hiyo waliafikiana kwa kauli moja kuwashirikisha wadau mbali mbali wakiwemo viongozi wa Nyumba Kumi na Makamishena wa Kaunti kulihusu ombi hilo kabla ya kutoa mwelekeo rasmi.

Mkutano wa Alhamisi ulihudhuriwa pia na Seneta wa Kaunti ya Kisumu Prof. Tom Ojenda SC, Seneta wa Kaunti ya Pokot Magharibi Julius Murgor, Seneta wa Kaunti ya Isiolo Fatuma Dullo na Seneta wa Kaunti ya Kajiado Seki Lenku.

The website encountered an unexpected error. Please try again later.